Wednesday, October 2, 2019

Naibu Waziri Kanyasu: Ujenzi Wa Bwawa La Kufua Umeme La Julius Nyerere Limezingatia Masuala Ya Usalama Wa Uhifadhi

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Constantine Kanyasu amesema nia ya Serikali ya ujenzi wa bwawa  la kufua umeme la Julius Nyerere iko pale pale na ujenzi wake unaendelea kwa kasi huku ukizingatia masuala ya Uhifadhi katika Pori la Akiba la Selous.

Akizungumza leo na Wabunge wa Kamati ya Bunge ya Mazingira, Uhifadhi wa Maliasili na Usalama wa Nyuklia kutoka Ujerumani Mhe. Kanyasu  amesema Tathmini ya Athari kwa Mazingira imefanyika na kuonyesha kuwa ujenzi huo ni salama katika shughuli za Uhifadhi.

“Serikali ya Awamu ya Tano inatekeleza mradi huu kwa kutumia fedha zake kutoka vyanzo vya ndani. Mradi huu utachukua eneo la ukubwa wa kilomita za  mraba 1,250 ambalo ni sawa na asilimia tatu (3%) tu ya eneo lote la pori la akiba selous lenye ukubwa wa kilomita za mraba 50,000.” Mhe. Kanyasu alisisitiza.

Mhe. Kanyasu amesema  kiwango cha umeme cha megawati 2,100 kitakachozalishwa katika gridi ya Taifa itasaidia kwa kiasi kikubwa kuokoa misitu inayokatwa kwa kasi kwa ajili ya nishati ya mkaa na kuni.

Aidha, Mhe. Kanyasu amewaeleza Wabunge hao kuwa ujio wa Bwawa hilo la Umeme limepelekea sehemu ya Pori la Akiba la Selous kupandishwa hadhi na kuwa Hifadhi ya Tiafa ya Julius Nyerere ambapo kufuatia hali hiyo ulinzi wa wanyamapori katika Hifadhi hiyo utakuwa madhubuti zaidi na ilivyokuwa mwanzo.

Katika hatua nyingine Mhe. Kanyasu amewaeleza Wabunge hao kuwa Serikali ya Tanzania imelichukua suala la mabadiliko ya tabia ya nchi kwa uzito unaostahili na kwa kutambua athari zake kwa mwaka huu imepandisha hadhi mapori ya akiba manne na  kuwa Hifadhi za Taifa na hivyo ulinzi wake wa Hifadhi hizo umeongezeka maradufu

Kwa upande wake Kiongozi wa ujumbe huo Mhe. Sylvia Kotting- Uhl ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa mageuzi makubwa yanayofanyika katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Tano katika masuala ya Uhifadhi  na kuahidi ushirikiano na nchi yake katika kujenga uwezo katika nyanja za kusimamia na kudhibiti taka za kielektroniki, Uzalishaji wa Umeme wa jua na kutoa mwaliko kwa ujumbe wa Tanzania kutembelea Ujerumani

Aidha, Mhe.Sylvia amesema licha ya ujenzi wa Bwawa la Umeme la Julius Nyerere bado wataendelea kuisaidia Serikali ya Tanzania katika masuala ya Uhifadhi kufuatia juhudi kubwa za Serikali ya awamu ya tano ya kuendelea kutunza na kuhifadhi maeneo yasiweze kuharibiwa na shughuli za kibinadamu.




from MPEKUZI https://ift.tt/2opfG5Z
via IFTTT

No comments:

Post a Comment