Saturday, October 5, 2019

RC Kagera Aongoza Mamia Ya Wananchi Mkoani Humo Kuboresha Taharifa Zao Kwenye Daftari La Wapiga Kura

Na Avitus Benedicto Kyaruzi, Kagera
Viongozi wa vyama vya siasa,watendaji na wananchi mkoani Kagera  wametakiwa kuweka umakini wa kipekee katika wilaya zote za mpakani ikiwemo Misenyi, Kyerwa, Ngara pamoja na Karagwe kuhakikisha kwamba hakuna mtu asiye na sifa anajipenyeza kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura.

Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Mkoa wa Kagera Brigedia Jenerali Marco Elisha Gaguti jana Oktoba 4, 2019 wakati akikagua  na kujionea hali halisi ya zoezi la uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura linaloendelea katika  vituo mbalimbali katika Manispaa ya Bukoba Mkoani Kagera.

Mkuu wa mkoa wa Kagera Brigedia Jenerali Marco Elisha Gaguti amesema hatarajii kuona mtu yoyote ambaye si raia wa Tanzania akishiriki katika zoezi hilo na endapo itatokea sheria na taratibu zitafuata mkondo wake kwa wote watakao kuwa wamehusika na jambo hilo kutokana na serikali kuwekeza fedha nyingi ili kuhakikisha wananchi wake wanapata fursa hiyo na wanatumia haki yao kikatiba kupata viongozi wanaohitaji kwa maendeleo ya taifa.

Aidha amefurahia muitikio mzuri wa wananchi wanaojitokeza katika uboreshaji wa daftari hilo na kutoa wito kwa wananchi wote katika maeneo yote ambayo yamewekwa vituo hivyo vya maboresho ya taarifa kutumia muda huo vizuri kuhakikisha wote wenye sifa za msingi za kupiga kura wafanye uboreshaji wa taarifa zao ili waweze kustahili kupiga kura katika uchaguzi mkuu ujao 2020.

Mkuu wa Mkoa wa Kagera pia amefanya uboreshaji wa kumbukumbu zake katika kituo cha kujiandikisha kilichopo katika kata ya Miembeni Manispaa ya Bukoba na kuwahimiza wananchi mkoani Kagera kutumia siku 7 za uboreshaji daftari la wapiga kura Oktoba 3 hadi Oktoba 9  kuhakikisha wamejiandikisha. 
 


from MPEKUZI https://ift.tt/2OlH53r
via IFTTT

No comments:

Post a Comment